Rukia maudhui

Mistari ya Biblia kuhusu Psalms

896 mistari · 16 vipengele

Mistari muhimu ya Biblia

Chuja kwa kitabu
  1. Inueni vichwa vyenu, enyi malango, inukeni enyi milango ya kale, ili mfalme wa utukufu apate kuingia.

  2. Ni nani huyu Mfalme wa utukufu? Ni Bwana aliye na nguvu na uweza, ni Bwana aliye hodari katika vita.

  3. Inueni vichwa vyenu, enyi malango, viinueni juu enyi milango ya kale, ili Mfalme wa utukufu apate kuingia.

  4. Ni nani yeye, huyu Mfalme wa utukufu? Ni Bwana Mwenye Nguvu Zote; yeye ndiye Mfalme wa utukufu.

  5. Zaburi ya Daudi. Ee Bwana, nithibitishe katika haki, maana nimeishi maisha yasiyo na lawama; nimemtumainia Bwana bila kusitasita.

  6. Ee Bwana, unijaribu, unipime, uuchunguze moyo wangu na mawazo yangu;

  7. kwa maana upendo wako uko mbele yangu daima, nami natembea siku zote katika kweli yako.

  8. Siketi pamoja na watu wadanganyifu, wala siandamani na wanafiki,

  9. ninachukia kusanyiko la watenda mabaya na ninakataa kuketi pamoja na waovu.

  10. Ninanawa mikono yangu kwa kuwa sina hatia, naikaribia madhabahu yako, Ee Bwana,

  11. nikitangaza sifa yako kwa sauti kubwa, huku nikisimulia matendo yako ya ajabu.

  12. Ee Bwana, naipenda nyumba yako mahali unakoishi, mahali ambapo utukufu wako hukaa.

  13. Usiiondoe nafsi yangu pamoja na watenda dhambi, wala uhai wangu pamoja na wamwagao damu,

  14. ambao mikononi mwao kuna mipango miovu, ambao mikono yao ya kuume imejaa rushwa.

  15. Bali mimi ninaishi maisha yasiyo na lawama; nikomboe na unihurumie.

  16. Miguu yangu imesimama katika uwanja tambarare; katika kusanyiko kuu nitamsifu Bwana.

  17. Zaburi ya Daudi. Bwana ni nuru yangu na wokovu wangu, nimwogope nani? Bwana ni ngome ya uzima wangu, nimhofu nani?

  18. Waovu watakaposogea dhidi yangu ili wanile nyama yangu, adui zangu na watesi wangu watakaponishambulia, watajikwaa na kuanguka.

  19. Hata jeshi linizunguke pande zote, moyo wangu hautaogopa; hata vita vitokee dhidi yangu, hata hapo nitakuwa na ujasiri.

  20. Jambo moja ninamwomba Bwana, hili ndilo ninalolitafuta: niweze kukaa nyumbani mwa Bwana siku zote za maisha yangu, niutazame uzuri wa Bwana na kumtafuta hekaluni mwake.

  21. Kwa kuwa siku ya shida, atanihifadhi salama katika maskani yake, atanificha uvulini mwa hema yake na kuniweka juu kwenye mwamba.

  22. Kisha kichwa changu kitainuliwa juu ya adui zangu wanaonizunguka. Katika maskani yake nitatoa dhabihu kwa kelele za shangwe; nitamwimbia Bwana na kumsifu.

  23. Isikie sauti yangu nikuitapo, Ee Bwana, unihurumie na unijibu.

  24. Moyo wangu unasema kuhusu wewe, “Utafute uso wake!” Uso wako, Bwana “Nitautafuta.”

  25. Usinifiche uso wako, usimkatae mtumishi wako kwa hasira; wewe umekuwa msaada wangu. Usinikatae wala usiniache, Ee Mungu Mwokozi wangu.