Rukia maudhui

Mistari ya Biblia kuhusu Psalms

896 mistari · 16 vipengele

Mistari muhimu ya Biblia

Chuja kwa kitabu
  1. Zaburi ya Daudi. Wakati alipokuwa katika Jangwa la Yuda. Ee Mungu, wewe ni Mungu wangu, nakutafuta kwa moyo wote; nafsi yangu inakuonea kiu, mwili wangu unakuonea wewe shauku, katika nchi kame na iliyochoka mahali ambapo hapana maji.

  2. Nimekuona katika mahali patakatifu na kuuona uwezo wako na utukufu wako.

  3. Kwa sababu upendo wako ni bora kuliko uhai, midomo yangu itakuadhimisha.

  4. Nitakusifu siku zote za maisha yangu, na kwa jina lako nitainua mikono yangu.

  5. Nafsi yangu itatoshelezwa kama kwa wingi wa vyakula; kwa midomo iimbayo kinywa changu kitakusifu wewe.

  6. Kitandani mwangu ninakukumbuka wewe, ninawaza juu yako makesha yote ya usiku.

  7. Kwa sababu wewe ndiwe msaada wangu, chini ya uvuli wa mbawa zako naimba.

  8. Nafsi yangu inaambatana nawe, mkono wako wa kuume hunishika.

  9. Wale wanaotafuta uhai wangu wataharibiwa, watakwenda chini kwenye vilindi vya dunia.

  10. Watatolewa wafe kwa upanga, nao watakuwa chakula cha mbweha.

  11. Bali mfalme atafurahi katika Mungu, wale wote waapao kwa jina la Mungu watamsifu, bali vinywa vya waongo vitanyamazishwa.

  12. Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi. Ee Mungu, unisikie ninapoeleza lalamiko langu, uyahifadhi maisha yangu kutokana na vitisho vya adui.

  13. Unifiche kutokana na shauri la siri la waovu, kutokana na zile kelele za kundi la watenda mabaya.

  14. Wananoa ndimi zao kama panga na kuelekeza maneno yao kama mishale ya kufisha.

  15. Hurusha mishale kutoka kwenye mavizio kwa mtu asiye na hatia, humrushia ghafula bila woga.

  16. Kila mmoja humtia moyo mwenzake katika mipango mibaya; huzungumza juu ya kuficha mitego yao, nao husema, “Ni nani ataiona?”

  17. Hufanya shauri baya la dhuluma na kusema, “Tumebuni mpango mkamilifu!” Hakika nia na moyo wa mwanadamu vina hila.

  18. Bali Mungu atawapiga kwa mishale, nao ghafula wataangushwa.

  19. Atageuza ndimi zao wenyewe dhidi yao na kuwaleta kwenye maangamizi; wote wawaonao watatikisa vichwa vyao kwa dharau.

  20. Wanadamu wote wataogopa, watatangaza kazi za Mungu na kutafakari yale aliyoyatenda.

  21. Wenye haki na wafurahi katika Bwana, na wakimbilie kwake; wanyofu wote wa moyo na wamsifu yeye!

  22. Kwa mwimbishaji. Zaburi ya Daudi. Wimbo. Ee Mungu, sifa zakungojea katika Sayuni; kwako wewe nadhiri zetu zitatimizwa.

  23. Ewe usikiaye maombi, kwako wewe watu wote watakuja.

  24. Tulipokuwa tumefunikwa kabisa na dhambi, wewe ulisamehe makosa yetu.

  25. Heri wale uliowachagua na kuwaleta karibu ili waishi katika nyua zako! Tunashibishwa kwa mema ya nyumba yako, mema ya Hekalu lako takatifu.