Mathayo 24:4-28
4
Yesu akawajibu, “Jihadharini, mtu yeyote asiwadanganye.
5
Kwa maana wengi watakuja kwa Jina langu, wakidai, ‘Mimi ndiye Kristo,’nao watawadanganya wengi.
6
Mtasikia habari za vita na matetesi ya vita. Angalieni msitishike, kwa maana haya hayana budi kutukia. Lakini ule mwisho bado.
7
Taifa litainuka dhidi ya taifa, na ufalme dhidi ya ufalme. Kutakuwa na njaa na mitetemeko ya ardhi sehemu mbalimbali.
8
Haya yote yatakuwa ndio mwanzo wa utungu.
9
“Ndipo mtasalitiwa, ili mteswe na kuuawa, nanyi mtachukiwa na mataifa yote kwa ajili yangu.
10
Wakati huo, wengi wataacha imani yao, nao watasalitiana kila mmoja na mwenzake na kuchukiana.
11
Watatokea manabii wengi wa uongo, nao watawadanganya watu wengi.
12
Kwa sababu ya kuongezeka kwa uovu upendo wa watu wengi utapoa,
13
lakini yule atakayevumilia hadi mwisho ataokolewa.
14
Injili ya Ufalme itahubiriwa ulimwenguni kote kuwa ushuhuda kwa mataifa yote. Ndipo mwisho utakapokuja.
15
“Hivyo mtakapoona lile ‘chukizo la uharibifu’ lililonenwa na nabii Danieli limesimama mahali patakatifu (asomaye na afahamu),
16
basi wale walioko Uyahudi wakimbilie milimani.
17
Yeyote aliye juu ya dari ya nyumba asishuke ili kuchukua chochote kutoka ndani ya nyumba.
18
Aliye shambani asirudi nyumbani kuchukua vazi lake.
19
Ole wao wenye mimba na wale wanaonyonyesha watoto siku hizo!
20
Ombeni ili kukimbia kwenu kusiwe wakati wa baridi au siku ya Sabato.
21
Kwa maana wakati huo kutakuwa na dhiki kuu ambayo haijapata kuwako tangu mwanzo wa dunia mpaka sasa: wala haitakuwako tena kamwe.
22
Kama siku hizo zisingefupishwa, hakuna hata mtu mmoja ambaye angeokoka. Lakini kwa ajili ya wateule, siku hizo zitafupizwa.
23
Wakati huo kama mtu yeyote akiwaambia, ‘Tazama, Kristo huyu hapa!’ Au, ‘Kristo yuko kule,’ msisadiki.
24
Kwa maana watatokea makristo wa uongo na manabii wa uongo, nao watafanya ishara kubwa na maajabu mengi ili kuwapotosha, ikiwezekana, hata wale wateule hasa.
25
Angalieni, nimekwisha kuwaambia mapema.
26
“Kwa hiyo mtu yeyote akiwaambia, ‘Yule kule nyikani,’ msiende huko. Au akisema, ‘Yuko kwenye chumba,’ msisadiki.
27
Kwa maana kama vile umeme utokeavyo mashariki na kuonekana hata magharibi, ndivyo itakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu.
28
Kwa maana popote ulipo mzoga, huko ndiko wakusanyikapo tai.
Settings