Skip to content

Mistari ya Biblia kuhusu Balaam

29 mistari · 8 vipengele

Mistari muhimu ya Biblia

Chuja kwa kitabu
  1. akatuma wajumbe kwenda kumwita Balaamu mwana wa Beori, ambaye alikuwa huko Pethori, karibu na Mto Frati, katika nchi yake ya kuzaliwa. Balaki akasema: “Taifa limekuja kutoka Misri, nao wamefunika uso wa nchi, nao wametua karibu nami.

  2. Sasa uje kuwalaani watu hawa, kwa kuwa wana nguvu sana kuniliko. Kisha huenda nikaweza kuwashinda na kuwatoa nje ya nchi. Kwa kuwa ninajua kwamba, wale unaowabariki wanabarikiwa na wale unaowalaani wanalaaniwa.”

  3. Wazee wa Moabu na wa Midiani wakaondoka, wakiwa wamechukua ada ya uaguzi. Walipokwenda kwa Balaamu, wakamweleza kile Balaki alikuwa amesema.

  4. Lakini Mungu alikasirika sana alipokwenda, naye malaika wa Bwana akasimama barabarani kumpinga. Balaamu alikuwa amepanda punda wake, na watumishi wake wawili walikuwa pamoja naye.

  5. Wakati punda alipomwona malaika wa Bwana akiwa amesimama barabarani akiwa na upanga uliofutwa mkononi mwake, punda akageukia upande kuelekea shambani. Balaamu akampiga ili amrudishe barabarani.

  6. Ndipo malaika wa Bwana akasimama katika njia nyembamba iliyo kati ya mashamba mawili ya mizabibu, yakiwa na kuta pande zote mbili.

  7. Punda alipomwona malaika wa Bwana, alijisukumiza karibu na ukuta, na kugandamiza mguu wa Balaamu ukutani. Ndipo Balaamu akampiga tena punda.

  8. Kisha malaika wa Bwana akaendelea mbele na kusimama mahali pembamba ambapo hapakuwepo nafasi ya kugeuka, upande wa kulia wala wa kushoto.

  9. Punda alipomwona malaika wa Bwana, alilala chini Balaamu angali amempanda, naye Balaamu akakasirika na kumpiga kwa fimbo yake.

  10. Kisha Bwana akakifungua kinywa cha punda, akamwambia Balaamu, “Nimekutendea nini kinachokufanya unipige mara hizi tatu?”

  11. Balaamu akamjibu punda, “Umenifanya mjinga! Kama ningelikuwa na upanga mkononi mwangu, ningelikuua sasa hivi.”

  12. Punda akamwambia Balaamu, “Je, mimi si punda wako mwenyewe, ambaye umenipanda siku zote, hadi leo? Je, nimekuwa na tabia ya kufanya hivi kwako?” Akajibu, “Hapana.”

  13. Kisha Bwana akafungua macho ya Balaamu, naye akamwona malaika wa Bwana amesimama barabarani akiwa ameufuta upanga wake. Balaamu akainama, akaanguka kifudifudi.

  14. Malaika wa Bwana akamuuliza Balaamu, “Kwa nini umempiga punda wako mara tatu hizi? Nimekuja kukuzuia kwa sababu njia yako imepotoka mbele yangu.

  15. Punda aliniona na kunikwepa mara hizi tatu. Kama punda hangenikwepa, hakika ningekuwa nimeshakuua sasa, lakini ningemwacha punda hai.”

  16. Balaamu akamwambia malaika wa Bwana, “Nimetenda dhambi. Sikutambua kuwa umesimama barabarani kunizuia. Basi kama haikupendezi, nitarudi.”

  17. Malaika wa Bwana akamwambia Balaamu, “Uende na watu hao, lakini useme tu lile nikuambialo.” Kwa hiyo Balaamu akaenda na wale wakuu wa Balaki.

  18. Balaamu alipotazama nje na kuona Israeli amepiga kambi kabila kwa kabila, Roho wa Mungu akawa juu yake,

  19. naye akatoa ujumbe wake: “Ujumbe wa Balaamu mwana wa Beori, ujumbe wake yeye ambaye jicho lake linaona vizuri;

  20. ujumbe wake yeye ambaye husikia maneno ya Mungu, ambaye huona maono kutoka kwa Mwenyezi, ambaye huanguka kifudifudi, na ambaye macho yake yamefunguka:

  21. “Tazama jinsi yalivyo mazuri mahema yako, ee Yakobo, maskani yako, ee Israeli!

  22. “Kama mabonde, yanaenea, kama bustani kando ya mto, kama miti ya udi iliyopandwa na Bwana, kama mierezi kando ya maji.

  23. Maji yatatiririka kutoka ndoo zake; mbegu yake itakuwa na maji tele. “Mfalme wake atakuwa mkuu kuliko Mfalme Agagi; ufalme wake utatukuka.

  24. “Mungu alimleta kutoka Misri; yeye ana nguvu kama nyati. Anayararua mataifa yaliyo adui zake, na kuvunja mifupa yao vipande vipande; huwachoma kwa mishale yake.

  25. Hujikunyata na kuvizia kama simba, kama simba jike; nani anayethubutu kumwamsha? “Abarikiwe kila akubarikiye, na alaaniwe kila akulaaniye!”