Kumbukumbu 2:24-37
24
“Ondoka sasa na uvuke Bonde la Arnoni. Tazama, nimemweka mikononi mwako Sihoni Mwamori, mfalme wa Heshboni na nchi yake. Anza kuimiliki nchi hiyo na umwingize katika vita.
25
Siku hii ya leo nitaanza kuwatia hofu na woga mataifa yote chini ya mbingu wawaogope ninyi. Watakaposikia taarifa zenu, watatetemeka na kufadhaika kwa sababu yenu.”
26
Kutoka jangwa la Kedemothi nilituma wajumbe wenye maneno ya amani kwa Sihoni mfalme wa Heshboni kusema,
27
“Turuhusu tupite katika nchi yako. Tutapita katika barabara kuu, hatutageuka kuume wala kushoto.
28
Tuuzie chakula tule na maji tunywe kwa thamani yake katika fedha. Turuhusu tu tupite kwa miguu,
29
kama wazao wa Esau ambao wanaishi Seiri na Wamoabu ambao wanaishi Ari walivyotufanyia, mpaka tuvuke Yordani kuingia nchi ambayo Bwana Mungu wetu anatupatia.”
30
Lakini Sihoni mfalme wa Heshboni alikataa kuturuhusu kupita. Kwa kuwa Bwana Mungu wako alikuwa ameifanya roho yake kuwa ngumu na moyo wake kuwa mkaidi ili amweke kwenye mikono yenu, kama alivyofanya sasa.
31
Bwana akaniambia, “Tazama, nimeanza kuwapa Mfalme Sihoni na nchi yake kwako. Sasa anzeni kuishinda na kuimiliki nchi yake.”
32
Wakati Sihoni pamoja na jeshi lake lote walipokuja kukutana nasi katika vita huko Yahazi,
33
Bwana Mungu wetu alimweka mikononi mwetu, nasi tukamwangamiza pamoja na wanawe na jeshi lake lote.
34
Kwa wakati ule tuliteka miji yake yote na kuiangamiza kabisa: wanaume, wanawake na watoto. Hatukumwacha yeyote.
35
Lakini mifugo na nyara tulizoziteka kutoka ile miji tulijichukulia wenyewe.
36
Kutoka Aroeri kwenye ukingo wa Bonde la Arnoni, kutoka mji ulio ndani ya bonde, hata mpaka Gileadi, hapakuwa na mji hata mmoja uliokuwa na nguvu kutushinda. Bwana Mungu wetu alitupa yote.
37
Lakini kulingana na amri ya Bwana Mungu wetu, hamkujiingiza katika nchi yoyote ya Waamoni, wala katika sehemu yoyote iliyo kandokando ya Mto Yaboki, wala katika miji iliyoko katika vilima.
Settings