Rukia maudhui

Isaya13

Ujumbe Juu ya Babeli

1
Neno kuhusu Babeli ambalo Isaya mwana wa Amozi aliliona:
2
Twekeni bendera juu ya mlima usio na kitu, wapazieni sauti, wapungieni mkono waingie katika malango ya wenye heshima.
3
Nimewaamuru watakatifu wangu; nimewaita mashujaa wangu waitimize hasira yangu: wale wanaoshangilia ushindi wangu.
4
Sikilizeni kelele juu ya milima, kama ile ya umati mkubwa wa watu! Sikilizeni, makelele katikati ya falme, kama mataifa yanayokusanyika pamoja! Bwana Mwenye Nguvu Zote anakusanya jeshi kwa ajili ya vita.
5
Wanakuja kutoka nchi za mbali sana, kutoka miisho ya mbingu, Bwana na silaha za ghadhabu yake, kuangamiza nchi yote.

Hofu ya Siku ya Bwana

6
Ombolezeni, kwa maana siku ya Bwana i karibu, itakuja kama uharibifu kutoka kwa Mwenyezi.
7
Kwa sababu ya hili, mikono yote italegea, moyo wa kila mtu utayeyuka.
8
Hofu itawakamata, uchungu na maumivu makali yatawashika, watagaagaa kama mwanamke aliye na utungu wa kuzaa. Watatazamana kwa hofu kila mtu na mwenzake, nyuso zao zikiwaka kama moto.
9
Tazameni, siku ya Bwana inakuja, siku katili, yenye ghadhabu na hasira kali, kuifanya nchi kuwa ukiwa na kuwaangamiza wenye dhambi waliomo ndani yake.
10
Nyota za mbinguni na makundi ya nyota havitatoa mwanga wake. Jua linalochomoza litatiwa giza na mwezi hautatoa nuru yake.
11
Nitauadhibu ulimwengu kwa ajili ya uovu wake, waovu kwa ajili ya dhambi zao. Nitakomesha majivuno ya wenye kiburi, na nitakishusha kiburi cha watu wakatili.
12
Nitawafanya wanadamu kuwa adimu kuliko dhahabu safi, watakuwa wachache sana kuliko dhahabu ya Ofiri.
13
Kwa hiyo nitazifanya mbingu zitetemeke, nayo dunia itatikisika kutoka mahali pake katika ghadhabu ya Bwana Mwenye Nguvu Zote, katika siku ya hasira yake iwakayo.
14
Kama swala awindwaye, kama kondoo wasio na mchungaji, kila mmoja atarudi kwa watu wake mwenyewe, kila mmoja atakimbilia nchi yake ya kuzaliwa.
15
Yeyote atakayetekwa atapasuliwa tumbo, wote watakaokamatwa watauawa kwa upanga.
16
Watoto wao wachanga watavunjwa vipande vipande mbele ya macho yao; nyumba zao zitatekwa na wake zao watatendwa jeuri.

Utekelezaji wa Hukumu kwa Wamedi

17
Tazama, nitawachochea Wamedi dhidi yao, ambao hawajali fedha wala hawafurahii dhahabu.
18
Mishale yao itawaangusha vijana, hawatakuwa na huruma kwa watoto wachanga wala hawataangalia watoto kwa huruma.

Ukiwa wa Milele wa Babeli

19
Babeli, johari ya falme, utukufu wa kiburi cha Wababeli, itaangushwa na Mungu kama Sodoma na Gomora.
20
Hautakaliwa na watu kamwe wala watu hawataishi humo kwa vizazi vyote. Hakuna Mwarabu atakayepiga hema lake huko, hakuna mchungaji atakayepumzisha makundi yake huko.
21
Lakini viumbe wa jangwani watalala huko, mbweha watajaza nyumba zake, bundi wataishi humo nao mbuzi-mwitu watarukaruka humo.
22
Fisi watalia ndani ya ngome zake, mbweha ndani ya majumba yake ya kifahari. Wakati wake umewadia, na siku zake hazitaongezwa.
Use arrow keys to navigate
Settings

Reading Style

Typeface

Font Size 19px

Reading Width 45 chars

Options