Skip to content
Hesabu 16:1-17

Hesabu 16:1-17

1
Kora mwana wa Ishari, mwana wa Kohathi, mwana wa Lawi, pamoja na baadhi ya Wareubeni, yaani Dathani na Abiramu, wana wa Eliabu, na Oni mwana wa Pelethi, wakachukua baadhi ya watu,
2
wakainuka dhidi ya Mose. Pamoja nao walikuwepo wanaume wa Kiisraeli 250, watu waliojulikana, viongozi wa jumuiya waliokuwa wameteuliwa kuwa wakuu wa kusanyiko.
3
Wakaja kama kikundi kuwapinga Mose na Aroni, wakawaambia, “Ninyi mmejitukuza sana! Kusanyiko hili lote ni takatifu, kila mmoja wao, naye Bwana yu pamoja nao. Kwa nini basi mmejitukuza wenyewe juu ya kusanyiko la Bwana?”
4
Mose aliposikia jambo hili, akaanguka kifudifudi.
5
Kisha akamwambia Kora na wafuasi wake wote: “Asubuhi Bwana ataonyesha ni nani aliye wake na ni nani aliye mtakatifu, tena atamtaka mtu huyo aje kwake. Mtu yule ambaye atamchagua atamfanya kuja karibu naye.
6
Wewe Kora na wafuasi wako wote mtafanya hivi: Chukueni vyetezo,
7
kesho wekeni moto na uvumba kwenye hivyo vyetezo mbele za Bwana. Mtu ambaye Bwana atamchagua atakuwa ndiye mtakatifu. Ninyi Walawi mmejitukuza sana!”
8
Pia Mose akamwambia Kora, “Enyi Walawi! Sasa nisikilizeni.
9
Haiwatoshi ninyi kwamba Mungu wa Israeli amewateua ninyi kutoka kusanyiko lote la Kiisraeli, na kuwaleta karibu naye mpate kufanya kazi kwenye Maskani ya Bwana, na kusimama mbele ya kusanyiko ili kuwahudumia?
10
Amekuleta wewe na ndugu zako Walawi mwe karibu naye, lakini sasa unajaribu kupata na ukuhani pia.
11
Wewe na wafuasi wako wote mmekusanyika pamoja kinyume cha Bwana. Aroni ni nani kwamba ninyi mnungʼunike dhidi yake?”
12
Kisha Mose akawaita Dathani na Abiramu, wana wa Eliabu. Lakini wao wakasema, “Sisi hatuji!
13
Haitoshi tu kwamba wewe umetuleta kutoka nchi itiririkayo maziwa na asali ili kutuua sisi jangwani? Nawe sasa pia unataka kuwa mkuu juu yetu?
14
Zaidi ya hayo, hujatuingiza katika nchi inayotiririka maziwa na asali, wala hujatupa urithi wa mashamba na mashamba ya mizabibu. Je, utayangʼoa macho ya watu hawa? Hapana, sisi hatuji!”
15
Ndipo Mose akakasirika sana na kumwambia Bwana, “Usiikubali sadaka yao. Mimi sikuchukua chochote, hata punda kutoka kwao, wala sijamkosea hata mmoja wao.”
16
Mose akamwambia Kora, “Wewe na wafuasi wako wote kesho mtatokea mbele za Bwana: yaani wewe na hao wenzako, pamoja na Aroni.
17
Kila mtu atachukua chetezo chake na kuweka uvumba ndani yake, vyetezo 250 kwa jumla, na kukileta mbele za Bwana. Wewe na Aroni mtaleta vyetezo vyenu pia.”
Settings

Reading Style

Typeface

Font Size 19px

Options