Waamuzi 11:30-40
30
Naye Yefta akaweka nadhiri mbele za Bwana akisema, “Ikiwa utawatia Waamoni mikononi mwangu,
31
chochote kile kitakachotoka katika mlango wa nyumba yangu cha kwanza ili kunilaki nirudipo kwa amani katika kuwashinda Waamoni, kitakuwa ni cha Bwana na nitakitoa kuwa sadaka ya kuteketezwa.”
32
Ndipo Yefta akavuka kupigana na hao Waamoni, naye Bwana akawatia mkononi mwake.
33
Akawapiga kwa ushindi mkubwa kuanzia Aroeri mpaka karibu na Minithi na kuendelea mpaka Abel-Keramimu, miji yote iliyopigwa ni ishirini. Basi Israeli wakawashinda Waamoni.
34
Yefta aliporudi nyumbani Mispa, tazama, binti yake akatoka ili kumlaki kwa matari na kucheza. Alikuwa ndiye mtoto pekee, hakuwa na mwana wala binti mwingine.
35
Alipomwona akararua mavazi yake akalia, “Ee! Binti yangu! Umenifanya niwe na huzuni na kunyongʼonyea sana, kwa kuwa nimeweka nadhiri kwa Bwana, ambayo siwezi kuivunja.”
36
Akajibu, “Baba yangu, umetoa neno lako kwa Bwana. Nitendee mimi kama vile ulivyoahidi, kwa kuwa Bwana amekupa ushindi dhidi ya adui zako Waamoni.”
37
Naye akamwambia baba yake, “Naomba nifanyiwe jambo hili. Nipewe miezi miwili ili kuzunguka vilimani nikaulilie ubikira wangu, mimi na wenzangu.”
38
Baba yake akamwambia, “Waweza kwenda.” Naye akamwacha aende kwa miezi miwili. Hivyo akaondoka pamoja na wasichana wenzake, naye akaulilia ubikira wake huko vilimani kwa sababu asingeolewa kamwe.
39
Baada ya hiyo miezi miwili, alirejea kwa baba yake, naye baba yake akamtendea kama alivyokuwa ametoa nadhiri yake. Naye alikuwa bikira. Nayo ikawa desturi katika Israeli,
40
kwamba kila mwaka binti wa Israeli huenda kwa siku nne ili kumkumbuka huyo binti wa Yefta, Mgileadi.
Settings