Skip to content
2 Wafalme 3:6-20

2 Wafalme 3:6-20

6
Kwa hiyo wakati ule Mfalme Yehoramu akaondoka kutoka Samaria na kukusanya Israeli yote tayari kwenda vitani.
7
Akapeleka pia ujumbe ufuatao kwa Yehoshafati mfalme wa Yuda: “Mfalme wa Moabu ameasi dhidi yangu. Je, utakwenda pamoja nami kupigana dhidi ya Moabu?” Akajibu, “Nitakwenda pamoja nawe. Mimi ni kama wewe, watu wangu ni kama watu wako, farasi wangu ni kama farasi wako.”
8
Akauliza, “Je, tutashambulia kupitia njia gani?” Akajibu, “Kupitia Jangwa la Edomu.”
9
Hivyo mfalme wa Israeli akaondoka akiwa pamoja na mfalme wa Yuda na mfalme wa Edomu. Baada ya kuzunguka kwa siku saba, jeshi likawa limeishiwa maji kwa matumizi yao na kwa ajili ya wanyama waliokuwa nao.
10
Mfalme wa Israeli akamaka, “Nini! Je, Bwana ametuita sisi wafalme watatu ili tu kututia mikononi mwa Moabu?”
11
Lakini Yehoshafati akauliza, “Je, hayuko nabii wa Bwana hapa, ili tuweze kumuuliza Bwana kupitia kwake?” Afisa mmoja wa mfalme wa Israeli akajibu, “Elisha mwana wa Shafati yuko hapa. Ndiye alikuwa akimimina maji juu ya mikono ya Eliya.”
12
Yehoshafati akasema, “Neno la Bwana liko pamoja naye.” Kwa hiyo mfalme wa Israeli na Yehoshafati pamoja na mfalme wa Edomu wakamwendea.
13
Elisha akamwambia mfalme wa Israeli, “Nina nini mimi nawe? Nenda kwa manabii wa baba yako na manabii wa mama yako.” Mfalme wa Israeli akajibu, “La hasha, kwa sababu ni Bwana ambaye ametuita pamoja sisi wafalme watatu ili atutie mikononi mwa Moabu.”
14
Elisha akasema, “Hakika, kama Bwana Mwenye Nguvu Zote aishivyo ambaye ninamtumikia, kama si kuheshimu Yehoshafati mfalme wa Yuda, nisingekutazama wala hata kukutupia jicho.
15
Lakini sasa, nileteeni mpiga kinubi.” Mpiga kinubi alipokuwa akipiga, mkono wa Bwana ukaja juu ya Elisha,
16
naye akasema, “Hivi ndivyo asemavyo Bwana, ‘Chimbeni bonde hili lijae mahandaki.’
17
Kwa kuwa hivi ndivyo asemavyo Bwana: Hamtaona upepo wala mvua, lakini bonde hili litajaa maji, nanyi pamoja na ngʼombe wenu na wanyama wenu wengine mtakunywa.
18
Hili ni jambo rahisi machoni pa Bwana. Pia ataitia Moabu mikononi mwenu.
19
Mtaushinda kila mji wenye ngome na kila mji mkubwa. Mtakata kila mti ulio mzuri, mtaziba chemchemi zote, na kuharibu kila shamba zuri kwa mawe.”
20
Kesho yake asubuhi, karibu na wakati wa kutoa dhabihu ya asubuhi, tazama, maji yakawa yanatiririka kutoka upande wa Edomu! Nayo nchi ikajaa maji.
Settings

Reading Style

Typeface

Font Size 19px

Options