Skip to content
2 Nyakati 35:1-14

2 Nyakati 35:1-14

1
Yosia akaadhimisha Pasaka kwa Bwana katika Yerusalemu, mwana-kondoo wa Pasaka akachinjwa siku ya kumi na nne ya mwezi wa kwanza.
2
Akawaweka makuhani kwenye wajibu wao na kuwatia moyo katika utumishi wa Hekalu la Bwana.
3
Akawaambia Walawi, waliowafundisha Waisraeli wote na waliokuwa wamejiweka wakfu kwa ajili ya kazi ya Bwana, “Liwekeni hilo Sanduku takatifu katika Hekalu lile alilojenga Solomoni mwana wa Daudi mfalme wa Israeli. Halipaswi kubebwa huku na huko mabegani mwenu. Sasa mtumikieni Bwana Mungu wenu na watu wake Israeli.
4
Jiandaeni kwa kufuata jamaa zenu katika migawanyo yenu, kufuatana na maelezo yaliyoandikwa na Daudi mfalme wa Israeli na mwanawe Solomoni.
5
“Simameni mahali patakatifu kwa kufuata migawanyo ya jamaa za baba zenu kulingana na koo zenu na pawepo Walawi kwa ajili ya kila mgawanyo wa nyumba ya baba zenu.
6
Chinjeni mwana-kondoo wa Pasaka, jitakaseni, nanyi kwa niaba ya koo zenu fanyeni maandalizi, mkitenda sawasawa na neno la Bwana kwa mkono wa Mose.”
7
Ndipo Yosia akawapa watu wote wana-mbuzi waliokuwepo jumla ya kondoo wapatao 30,000 kwa ajili ya sadaka ya Pasaka, pia na ngʼombe 10,000, vyote hivi kutoka mali binafsi ya mfalme.
8
Pia maafisa wake, wakatoa kwa hiari yao wakawapa watu, makuhani na Walawi. Hilkia, Zekaria na Yehieli, waliokuwa maafisa wakuu wa Hekalu la Mungu, wakawapa makuhani sadaka za Pasaka wana-kondoo na wana-mbuzi 2,600 na mafahali 300.
9
Konania na nduguze wawili, Shemaya na Nethaneli, pamoja na Hashabia, Yeieli na Yozabadi waliokuwa viongozi wa Walawi, nao pia wakawapa Walawi wana-kondoo na wana-mbuzi 5,000 na mafahali 500, kwa ajili ya sadaka za Pasaka.
10
Huduma ilipomalizika kuandaliwa makuhani wakasimama mahali pao na Walawi katika migawanyo yao kama mfalme alivyokuwa ameamuru.
11
Wana-kondoo wa Pasaka wakachinjwa, nao makuhani wakanyunyiza ile damu waliyokabidhiwa, wakati Walawi wakiwa wanawachuna wale wanyama ngozi.
12
Wakatenga sadaka za kuteketezwa ili waweze kugawia ili migawanyo kwa kufuata jamaa za baba zao ili watoe sadaka kwa Bwana kama ilivyoandikwa katika Kitabu cha Mose. Wakafanya vivyo hivyo kwa wale mafahali.
13
Wakawaoka wale wanyama wa Pasaka kwenye moto kama ilivyoamriwa, wakachemsha zile sadaka takatifu kwenye vyungu, masufuria makubwa na vikaango na kuwagawia watu wote upesi.
14
Hatimaye wakafanya maandalizi kwa ajili yao wenyewe na kwa ajili ya makuhani, kwa sababu wale makuhani, yaani, wazao wa Aroni, walikuwa wanatoa sadaka za kuteketezwa pamoja na zile sehemu zilizonona mpaka usiku. Hivyo Walawi wakafanya maandalizi kwa ajili yao wenyewe na kwa ajili ya makuhani wa uzao wa Aroni.
Settings

Reading Style

Typeface

Font Size 19px

Options