Mika 4:1-8
1
Katika siku za mwisho mlima wa Hekalu la Bwana utaimarishwa kama mlima mkuu miongoni mwa milima yote; utainuliwa juu ya vilima, na watu wa mataifa watamiminika humo.
2
Mataifa mengi yatakuja na kusema, “Njooni, twendeni mlimani mwa Bwana, kwenye nyumba ya Mungu wa Yakobo. Atatufundisha njia zake, ili tuweze kuenenda katika mapito yake.” Sheria itatoka Sayuni, neno la Bwana litatoka Yerusalemu.
3
Atahukumu kati ya mataifa mengi, na ataamua migogoro ya mataifa yenye nguvu na yaliyo mbali. Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao kuwa miundu ya kukata matawi. Taifa halitainua upanga dhidi ya taifa jingine, wala hawatajifunza vita tena.
4
Kila mtu ataketi chini ya mzabibu wake na chini ya mtini wake, wala hakuna mtu atakayewaogopesha, kwa kuwa Bwana Mwenye Nguvu Zote amesema.
5
Mataifa yote yanaweza kutembea katika jina la miungu yao; sisi tutatembea katika jina la Bwana Mungu wetu milele na milele.
6
“Katika siku hiyo,” asema Bwana, “nitawakusanya walemavu; nitawakusanya walio uhamishoni na wale niliowahuzunisha.
7
Nitawafanya walemavu kuwa mabaki, wale waliofukuzwa kuwa taifa lenye nguvu. Bwana atatawala juu yao katika Mlima Sayuni kuanzia siku hiyo na hata milele.
8
Lakini kuhusu wewe, ee mnara wa ulinzi wa kundi, ee ngome ya Binti Sayuni, milki ya awali itarudishwa kwako, ufalme utakuja kwa Binti Yerusalemu.”
Settings