Waamuzi 13:15-23
15
Manoa akamjibu yule malaika wa Bwana, “Twakuomba usubiri kwanza ili tuweze kuandaa mwana-mbuzi kwa ajili yako.”
16
Malaika wa Bwana akamjibu, “Hata kama utanizuia, sitakula chochote kwako. Lakini ukitaka kuandaa sadaka ya kuteketezwa, mtolee Bwana hiyo sadaka.” (Kwa kuwa Manoa hakujua kuwa alikuwa malaika wa Bwana.)
17
Ndipo Manoa akamuuliza yule malaika wa Bwana, “Jina lako ni nani, ili kwamba tuweze kukupa heshima hapo hayo uliyonena yatakapotimia?”
18
Akamjibu, “Kwa nini unauliza Jina langu? Ni Jina la ajabu.”
19
Ndipo Manoa akamchukua mwana-mbuzi, pamoja na sadaka ya unga, naye akamtolea Bwana dhabihu hapo juu ya mwamba. Naye yule malaika wa Bwana akafanya jambo la ajabu wakati Manoa na mkewe wakiwa wanaangalia:
20
Mwali wa moto kutoka hapo madhabahuni ulipowaka kuelekea mbinguni, malaika wa Bwana akapaa ndani ya huo mwali. Manoa na mkewe, kwa kuona jambo hili, wakaanguka chini kifudifudi.
21
Malaika wa Bwana hakumtokea tena Manoa na mkewe. Ndipo Manoa akatambua kuwa huyo alikuwa malaika wa Bwana.
22
Manoa akamwambia mkewe, “Hakika tutakufa, kwa kuwa tumemwona Mungu.”
23
Lakini mkewe akamwambia, “Ikiwa Bwana alikuwa amekusudia kutuua, asingelipokea sadaka ya kuteketezwa na sadaka ya unga kutoka mikononi mwetu, wala asingelituonyesha mambo haya yote wala kututangazia mambo kama haya wakati huu.”
Settings