Isaya 51:9-23
9
Amka, Amka! Jivike nguvu, ewe mkono wa Bwana, Amka, kama siku zilizopita, kama vile vizazi vya zamani. Si ni wewe uliyemkata Rahabu vipande vipande, uliyemchoma yule joka?
10
Si ni wewe uliyekausha bahari, maji ya kilindi kikuu, uliyefanya barabara katika vilindi vya bahari ili waliokombolewa wapate kuvuka?
11
Wale waliolipiwa fidia na Bwana watarudi. Wataingia Sayuni wakiimba; furaha ya milele itakuwa taji juu ya vichwa vyao. Furaha na shangwe zitawapata, huzuni na kulia kwa uchungu kutatoweka.
12
“Mimi, naam mimi, ndimi niwafarijie ninyi. Ninyi ni nani hata kuwaogopa wanadamu wanaokufa, wanadamu ambao ni majani tu,
13
kwamba mnamsahau Bwana Muumba wenu, aliyezitanda mbingu na kuiweka misingi ya dunia, kwamba mnaishi katika hofu siku zote kwa sababu ya ghadhabu ya mdhalimu, ambaye nia yake ni kuangamiza? Iko wapi basi ghadhabu ya mdhalimu?
14
Wafungwa waliojikunyata kwa hofu watawekwa huru karibuni; hawatafia kwenye gereza lao, wala hawatakosa chakula.
15
Kwa maana Mimi ndimi Bwana, Mungu wako, ambaye huisukasuka bahari ili mawimbi yake yangurume: Bwana Mwenye Nguvu Zote ndilo jina lake.
16
Nimeweka maneno yangu kinywani mwako na kukufunika kwa uvuli wa mkono wangu: Mimi niliyeweka mbingu mahali pake, niliyeweka misingi ya dunia, niwaambiaye Sayuni, ‘Ninyi ni watu wangu.’ ”
17
Amka, amka! Simama, ee Yerusalemu, wewe uliyekunywa kutoka mkono wa Bwana kikombe cha ghadhabu yake, wewe uliyekunywa mpaka kufikia machujo yake, kikombe kile cha kunywea kiwafanyacho watu kuyumbayumba.
18
Kati ya wana wote aliowazaa hakuwepo hata mmoja wa kumwongoza, kati ya wana wote aliowalea hakuwepo hata mmoja wa kumshika mkono.
19
Majanga haya mawili yamekuja juu yako: ni nani awezaye kukufariji? Maangamizi, uharibifu, njaa na upanga: ni nani awezaye kukutuliza?
20
Wana wako wamezimia, wamelala kwenye mwanzo wa kila barabara, kama swala aliyenaswa kwenye wavu. Wamejazwa na ghadhabu ya Bwana na makaripio ya Mungu wako.
21
Kwa hiyo sikiliza hili, wewe uliyeteswa, uliyelewa, lakini si kwa mvinyo.
22
Hili ndilo asemalo Bwana Mwenyezi wako, Mungu wako, yeye ambaye huwatetea watu wake: “Tazama, nimeondoa mkononi mwako kikombe kilichokufanya uyumbayumbe; kutoka kikombe hicho, kikombe cha kunywa cha ghadhabu yangu, kamwe hutakunywa tena.
23
Nitakiweka mikononi mwa watesi wako, wale waliokuambia, ‘Anguka kifudifudi ili tuweze kutembea juu yako.’ Ukaufanya mgongo wako kama ardhi, kama njia yao ya kupita.”
Settings